RAIS MAGUFULI AVIAGIZA VYOMBO VYA DOLA KUWACHUKULIA HATUA WATU WANAOTOA TAKWIMU ZA UONGO.

TAREHE 20-12-2017


Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mh John Magufuli ameviagiza vyombo vya dola hapa nchini kuwachukulia hatua kali za kisheria watu wote wanaotoa takwimu za uongo hapa nchini na kupotosha jamii kuhusu maendeleo ya nchi.

Mh Magufuli ametoa maagizo hayo leo muda mfupi kabla ya kuweka jiwe la msingi katika jengo la takwimu ya taifa lililopo mkoani Dodoma,ambapo amesema kuwa kulingana na kifungu namba 37 cha sheria za takwimu hapa nchini mtu anayetoa takwimu za uongo adhabu yake ni kifungo cha miezi sita hadi miaka mitatu au faini ya shilingi milioni kumi au adhabu zote kwa pamoja.

Amesema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakitoa takwimu za uongo kuhusu ukuaji wa uchumi kwa lengo la kukwamisha juhudi za serikali za kuwaletea wananchi wake maendeleo,hivyo kuanzia sasa mtu yeyote atakayebainika kutoa takwimu za uongo atashughulikiwa kwa mujibu wa sheria ya mwaka wa 2015.

Aidha Mh Magufuli ameongeza kuwa katika nusu ya kwanza ya mwaka huu takwimu zinaonesha kuwa uchumi wa Tanzania unaendelea kukua kwa asilimia 6.8 na kufanya Tanzania kuongoza katika nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki na pia ni miongoni mwa nchi tano barani Afrika ambazo uchumi wake unakuwa kwa kasi.


Kwa upande wake mkurugenzi mkuu wa ofisi ya taifa ya takwimu Dr Albina Chuwa amesema kuwa ofisi hiyo imekuwa ikifanya vizuri kimataifa,ambapo barani Afrika Tanzania imekuwa nchi ya pili katika kutoa takwimu bora ikitanguliwa na nchi ya Afrika Kusini kati ya nchi 54 za Afrika.
RAIS MAGUFULI AVIAGIZA VYOMBO VYA DOLA KUWACHUKULIA HATUA WATU WANAOTOA TAKWIMU ZA UONGO. RAIS MAGUFULI AVIAGIZA  VYOMBO VYA DOLA KUWACHUKULIA  HATUA WATU WANAOTOA TAKWIMU ZA UONGO. Reviewed by safina radio on December 20, 2017 Rating: 5

No comments